settings icon
share icon
Swali

Ni nini kinachofanya dhambi ya ngono kuwa jambo kubwa?

Jibu


Utamaduni wa kisasa umekuwa ukijaribu kufafanua upya mapenzi kama haki ya kibinafsi ya kutenda kwa njia yoyote mtu binafsi anavyotaka. Tabia ya ngono inachukuliwa kama chaguo la kibnafsi, kama vile uamuzi wa kununua nyumba au kukodisha. Wakati huo huo, maoni maarufu yameondoa neno dhambi katika msamiati wa utamaduni wetu. Usemi pekee wa ngono unaoonekana kuwa “mbaya” ni ule unaoonekana kuwa mbaya kwa mfafanuzi. Hata hivyo, kukubalika kijamii hutofautiana sana kiasi kwamba hata vitendo viovu zaidi viongeonekana kuwa vya haki kwa wengi. Kwa hiyo, kabla hatujaweza kuamua kwa nini dhambi ya ngono ni jambo kubwa, tunapaswa kufafanua dhambi ya ngono.

Kwa bahati nzuri, mwanadamu hajawahi kupewa fursa ya kufafanua dhambi. Yeye aliyeumba tendo la ndoa pia ana haki ya kuiwekea mipaka yake,na Biblia iko wazi kuhusu miongozo. Mungu alipomuumba mwanadamu wa kwanza,Adamu, na kumletea mwanamke wa kwanza, Hawa, Aliwaunganisha pamoja katika ndoa na kuitamka kuwa “nzuri”(Mwanzo 1:31;2:18, 24). Wakati huo, Mungu alianzisha tendo la ndoa na kuweka mipaka ya kuelezea kwake. Mungu aliumba muungano kati ya mume na mke ambao Aliuita “kuwa mwili mmoja” (Mwanzo 2:24; Mathayo 19:6; Marko 10:8; Waefeso 5:31). Kisha akafafanua shughuli yoyote ya ngono nje ya uhusiano wa mume-mke kuwa ukiukaji wa zawadi Yake. Uasherati, ushoga, ponografia, na tamaa ni ukiukaji wa nia ya Mungu alipoumba tendo la ndoa (1 Wakorintho 6:9, 18; Wagalatia 5:19-20; Yuda 1:7; Mathayo 5:28; Waebrania 13:4).

Basi kwa nini ukiukaji wa mipaka hiyo ni jambo kubwa? Kidokezo cha kwanza kiko katika Mwanzo 2:24 pamoja na maneno “mwili mmoja.” Kuna nguvu kubwa ya kuunganisha kwa kushiriki ngono. Mungu alikusudia ihusishe sio tu miili bali pia mioyo na maisha. Ngono ilikusudiwa kukamilisha umoja wa maisha kati ya mwanaume na mwanamke. Yesu alisema, “Alichokiungansiha Mungu, mwanadamu asikitenganishe” (Mathayo 19:6; Marko 10:9). Aliziumba miili ya mwanaume na mwanamke tofauti ili waweze kuja pamoja katika tendo la ukaribu wa kimwili linalowaunganisha pamoja kwa maisha. “Na hao wawili watakuwa mwili mmoja; hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja” (Marko 10:8). Tendo la kuwa mmoja huumba chombo kipya: familia. Nguvu hii kuu pia huzaa uhai mpya (Mwanzo 4:25). Kizazi cha binadamu kinaweza kuenezwa tu wakati mwanaume na mwanamke wanakuja pamoja. Na ndani ya ndoa, Mungu huibariki (Mwanzo 1:28; 9:27; Zaburi 17:3). Ngono ni zawadi kwa mume na mke ili kufanya uhusiano wao uwe wa kipekee kati ya mahusiano mengine yote.

Hata hivyo, kile Mungu anachokiumba kuwa chema, Shetani hupotosha. Shetani alianza kupotosha katika Bustani la Edeni kwa maneno “Je, Mungu amesema?” (Mwanzo 3:1). Na changamoto hiyo kwa mamlaka ya Mungu inaendelea bado. Tunapoitumia ngono kwa ajili ya burudani au kuridhisha tamaa, tunapunguza uzuri wa zawadi hii yenye nguvu na kumkufuru Yeye aliyeibuni. Sisi pia tunavuna matokeo ya dhambi. Kwa kutotii kwetu kingono kumetokeza ulimwengu ambao uko chini ya uzito wa magonjwa, uaviaji mimba, upotovu, ubakaji wa watoto, uraibu, na unyanyasaji wa kingono. Mungu aliweka mipaka kwa manufaa yetu ili tuweze kufurahia zawadi yake kama ilivyokusudiwa kufurahiwa.

Umeme ni kitu chenye nguvu na cha msaada mkubwa ikiwa unatumika ipasavyo. Hata hivyo, umeme ukitumika vibaya unaweza kusababisha kifo. Vivyo hivyo na ujinsia. Ikiwa unatumiwa vibaya, ngono pia ni mbaya. Kutumia vibaya zawadi ya Mungu huleta shida kama vile utoaji mimba, umasikini, ubakaji, uzinzi, talaka, na ponografia. Dhambi ya ngono huanza na majaribu, kama vile tu dhambi zingine. Tunapokataa kutambua mipaka ya Mungu, tunaruhusu tamaa kutawala chaguo zetu. Na tamaa kamwe haiwezi kuongoza katika mwelekeo sahihi. Yakobo 1:13-15 inasema, “Mtu ajaribiwapo, asiseme, Ninajaribiwa na Mungu; maana Mungu hawezi kujaribiwa na maovu, wala yeye mwenyewe hamjaribu mtu. Lakini kila mmoja hujaribiwa na tamaa yake mwenyewe huku akivutwa na kudanganywa. Halafu ile tamaa ikiisha kuchukua mimba huzaa dhambi, na ile dhambi ikiisha kukomaa huzaa mauti.”

Sababu nyingine dhambi ya ngono inachukuliwa kuwa kosa kubwa ni kwamba huharibu mfano wa agano lisilovunjika ambalo Mungu analo na watu wake. Biblia hutumia ndoa kama sitiari kuelezea uhusiano wa agano ambalo Yesu analo na “bi harusi” wake, wale ambao amewanunua kwa damu yake mwenyewe (Ufunuo 19:7; 2 Wakorintho 11:2). Katika Agano la kale, Mungu mara nyingi alifananisha Israeli ya kuasi na mke mpotovu, akitumia uzinzi kama mfano wa dhambi mbaya zaidi (Yeremia 3:6). Mungu aliumba tendo la ngono kuwa utimilifu wa uhusiano wa agano-agano ambalo Mungu ameshiriki (Malaki 2:14; Mathayo 19:6; Marko 10:9). Agano la ndoa linaonyesha agano lisilovunjika la Mungu nasi. Kushiriki katika ngono nje ya ndoa kunakiuka kusudi la Mungu na huleta matokeo mabaya.

Dhambi ya ngono huchafua zaidi ya miili yetu ya kimwili (1 Wakorintho 6:18). Ina umuhimu wa kiroho. Karibu kila kitabu cha Biblia hukataza uasherati, kuonyesha kwamba Mungu analiona kuwa ni dhambi kubwa. Kutenda dhambi ya ngono kunapingana moja kwa moja na mapenzi ya Mungu ya kututakasa (1 Wathesalonike 4:3).

Warumi 13:13-14 inaelezea maisha ambayo Mungu anataka tuishi: “Kama ilivyohusika na mchana na tuenende kwa adabu; si kwa ulafi na ulevi, si kwa ufisadi na uasherati, si kwa ugomvi na wivu. Bali mvaeni Bwana Yesu Kristo, wala msiuangalie mwili, hata kuwasha tamaa zake.” Dhambi ya ngono ni njia moja zaidi ambayo watu huridhisha mwili badala ya kutembea katika Roho (Wagalatia 5:16). Yesu alisema kwamba “wenye moyo safi” watamwona Mungu (Mathayo 5:8). Dhambi ya ngono isiyotubu huchafua moyo, na kuifanya iwe haiwezekani kupata nguvu za Roho Mtakatifu katika maisha yetu. Ikiwa tunataka kuwa na moyo safi, hatufai kufanya dhambi ya ngono.

English



Rudi kwa ukurasa wa nyumbani wa Kiswahili

Ni nini kinachofanya dhambi ya ngono kuwa jambo kubwa?
Shiriki ukurasa huu: Facebook icon Twitter icon Pinterest icon Email icon
© Copyright Got Questions Ministries