settings icon
share icon
Swali

Je, kutojua ni kisingizio cha kutosha cha dhambi?

Jibu


Ikiwa kwa “kisingizio” tunamaanisha kwamba kwa sababu ya kutojua kwetu Mungu atapuuza makosa yetu, basi hakuna visingizio vya kutosha vya dhambi. Dhambi ni wazo lolote, neno, au tendo linalofanywa na wanadamu ambalo linapingana na ukamilifu wa Mungu. Adamu na Hawa walipoumbwa mara ya kwanza, hawakufanya lolote lililopingana na ukamilifu wa Mungu (Mwanzo 1:27-31). Waliumbwa katika hali nzuri na kubaki bila dosari hadi walipokubali majaribu (Mwanzo 3:6-7). Inaweza kujadiliwa kwamba, kwa kuwa hawakuwahi kushuhudia kifo, hawakuwa wanajua uzito wa matokeo ya dhambi. Lakini hiyo haikuwa kisingizio cha dhambi yao.

Mungu alipowapa Waisraeli Sheria Yake, alijumuisha maagizo maalum kuhusu dhabihu wakati mtu, au taifa zima, alipotenda dhambi kwa kutojua (Waebrania 9:7). Mambo ya Walawi 4 inaelezea mpango wa Mungu kwa wale waliotenda dhambi bila kukusudia au kwa kutojua. Hesabu 15:22–29 inarudia mpango huu na inatoa maelezo kuhusu dhabihu maalum zinazohitajika ili kupata msamaha kutoka kwa Bwana wakati mtu alitenda dhambi kwa kutojua. Mambo ya Walawi 5:17 inasema wazi: “Na kama mtu akifanya dhambi, na kutenda mambo hayo mojawapo ambayo BWANA alizuilia yasifanywe, ajapokuwa hakuyajua, ni mwenye hatia vivyo, naye atachukua uovu wake.” Kutojua si sababu ya msamaha wa dhambi; dhambi ambazo Waisraeli walizitenda kwa kutojua bado zilihitaji dhabihu ya upatanisho.

Ingawa kutojua hakusamehi dhambi, kunaweza kupunguza adhabu. Adhabu ya Sheria kwa dhambi isiyo ya kukusudia ilikuwa nyepesi zaidi kuliko ile ya uasi wa makusudi au kufuru. Yesu alirudia kanuni hii katika Luka 12:47–48: “Na mtumwa Yule aliyejua mapenzi ya bwana wake, asijiweke tayari, wala kuyatenda mapenzi yake, atapigwa sana. Na Yule asiyejua, naye amefanya yastahiliyo mapigo, atapigwa kidogo. Na kila aliyepewa vingi, kwake huyo vitatakwa vingi; naye waliyemwekea amana vitu vingi, kwake huyo watataka na zaidi” (msisitizo umeongezwa).

Lazima tujifunze kuchukua dhambi kwa uzito jinsi Mungu anavyoichukua. Sababu moja ya dhabihu zote na mila ya utakaso katika Agano la Kale ilikuwa kuwaonyesha watu jinsi walivyo mbali na utakatifu wa Mungu. Kusudi la matokeo mabaya ni kutufundisha kuona dhambi jinsi Mungu anavyoiona na kuichukia jinsi anavyoichukia (Zaburi 31:6; Mithali 29:27). Tunapokuwa tunatenda dhambi kwa kutojua, Mungu huleta matokeo ili kutusaidia kujifunza. Mara tu tunapojua vizuri, anatarajia tufanye vizuri zaidi. Tunafanya vivyo hivyo kwa watoto wetu. Kwa kuwa mtoto wa miaka minne hakuwahi kuambiwa hasifinye ndizi dukani haimaanishi kuwa Mama yuko sawa nayo. Kutakuwa na matokeo, hata kama anaweza kudai kutojua sheria hiyo maalum, na ataambiwa wazi kuwa kufinya ndizi hakutavumiliwa tena. Bila shaka, matokeo yake mara ya kwanza huenda yasifikie ukali kama yatakavyokuwa endapo Mama angempata akifinya ndizi zaidi baada ya kuagizwa kutofanya hivyo.

Hata hivyo, madai mengi ya kutojua hayafai. Warumi 1:20 inasema kwamba hakuna udhuru wa kutokuamini uwepo wa Mungu: sifa zisizoonekana za Mungu “zinaonekana wazi” katika uumbaji. Mika 6:8 pia inakabiliana na madai yetu ya kutojua: “Ee mwanadamu, yeye amekuonyesha yaliyo mema; na BWANA anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako.” Ikiwa kutojua hakuondoi dhambi, basi kujifanya kutojua ni mbaya zaidi.

Mungu ni Baba, naye anawapenda watoto wake (Warumi 8:15). Hafurahii kutuadhibu sisi bali kutufanya tufanane na mfano wa Mwanawe (Warumi 8:29). Havumilii visingizio, ikiwemo kisingizio cha kutojua; badala yake, hutupatia fursa za kujifunza kutokana na matokeo yetu ili tufanye chaguo bora. Anajua kila mmoja wetu amepewa nini na hutufanya tuwajibike kwa kile tunachofanya nacho (Mathayo 13:11–12; Matendo 17:30). Sote tumetenda dhambi kwa kutojua, lakini Mungu hatuachi katika ujinga (1 Petro 1:14). Ametupa Neno lake ili kutuonyesha jinsi ya kuishi, naye anatarajia sisi kulitumia katika maisha yetu na kutafuta utakatifu, “ambao pasipo huo hakuna mtu atakayemwona Bwana” (Waebrania 12:14).

English



Rudi kwa ukurasa wa nyumbani wa Kiswahili

Je, kutojua ni kisingizio cha kutosha cha dhambi?
Shiriki ukurasa huu: Facebook icon Twitter icon Pinterest icon Email icon
© Copyright Got Questions Ministries