settings icon
share icon
Swali

Je, Biblia inafundisha kwamba kuna karama ya useja?

Jibu


Vifungu viwili katika Agano Jipya hutumiwa kujadili kile ambacho wakati mwingine huitwa “karama ya useja.” Cha kwanza ni Mathayo 19:9-12, “Mimi nawaambia, yeyote amwachaye mkewe isipokuwa kwa sababu ya uasherati naye akaoa mke mwingine, anazini. Naye amwoaye yule mwanamke aliyeachwa pia anazini.” Wanafunzi wake wakamwambia, “Kama hali ndiyo hii kati ya mume na mke, ni afadhali mtu asioe!” Yesu akawaambia, “Si watu wote wanaoweza kupokea neno hili, isipokuwa wale tu waliojaliwa na Mungu. Kwa maana wengine ni matowashi kwa sababu wamezaliwa hivyo; wengine wamefanywa matowashi na wanadamu; na wengine wamejifanya matowashi kwa ajili ya Ufalme wa Mbinguni. Yeye awezaye kulipokea neno hili na alipokee.”

Kifungu “isipokuwa wale tu waliojaliwa na Mungu” hurejelea watu wanaopokea kile ambacho wengine hukiita “karama ya useja” au “karama ya ukapera.” Licha ya kile tunachokiita karama, Yesu anafundisha kwamba watu wengi hawataki kwa kiasili kubaki waseja na useja maishani mwao yote. Isipokuwa ni wale ambao “wamekataa ndoa” kwa ajili ya ufalme. Waseja kama hao wamepokea zawadi ya pekee kutoka kwa Mungu.

Kifungu kingine kinachofaa ni 1 Wakorintho 7. Katika sura hii Paulo anasema kwamba si vibaya kuoa, lakini kwamba ni bora ikiwa Mkristo anaweza kukaa bila kuoa. (Sababu ni kwamba uangalifu wa mwanamume aliyefunga ndoa “unagawanywa” kati ya kumpendeza Bwana na kumpendeza mke wake; mwanamume mseja yuko huru kukazia fikira zaidi kazi ya Bwana, mistari ya 32-34.) Paulo anasema, “Laiti watu wangekuwa kama mimi nilivyo. Lakini kila mtu amepewa kipawa chake kutoka kwa Mungu, mmoja ana kipawa cha namna hii na mwingine ana cha namna ile” (mstari 7). Paulo ni mwangalifu katika kusema kwamba hiyo ni “kibali, si…amri” (mstari 6). Uwezo wa kukaa mseja na kumtumikia Mungu bila kufunga ndoa ni karama. Paulo na wengine walikuwa na karama hii, lakini si kila mtu.

Kama tunavyoona, Biblia haisemi waziwazi “karama ya useja” lakini inaonyesha kwamba uwezo wa kubaki bila kufunga ndoa ili kumtumikia Mungu kikamilifu zaidi ni karama. Watu wazima wengi wanatamani ndoa, na tamaa hii si dhambi. Kwa kweli, ndoa inaweza kutuepusha na dhambi: “Lakini ili kuepuka zinaa, kila mwanaume na awe na mke wake mwenyewe na kila mwanamke awe na mume wake mwenyewe” (1 Wakorintho 7:2). Badala ya kujihusisha katika uasherati, waumini wanapaswa kuoa. Ngono ndani ya ndoa kati ya mwanamume mmoja na mwanamke mmoja au useja— hizi ndizo chaguo mbili pekee kwa Wakristo.

Ingawa Biblia inazungumza kuhusu useja kama karama, haijaorodheshwa pamoja na karama za kiroho (1 Wakorintho 12; Warumi 12). Useja ni zawadi ambayo Mungu humpa kila mtu, angalau kwa muda. Kwa wengine, zawadi ya useja ni ya kudumu; kwa wengine, Mungu huchukua zawadi hiyo na kutoa zawadi ya ndoa mahali pake. Biblia inawatia moyo wale ambao ni waseja katika utumishi wa Kikristo kwamba wao ni sehemu muhimu ya familia ya Mungu.

English



Rudi kwa ukurasa wa nyumbani wa Kiswahili

Je, Biblia inafundisha kwamba kuna karama ya useja?
Shiriki ukurasa huu: Facebook icon Twitter icon Pinterest icon Email icon
© Copyright Got Questions Ministries