settings icon
share icon
Swali

Je! Tutakula chakula mbinguni?

Jibu


Watu wengi huuliza kama tutakula chukula mbinguni kwa sababu kula sio muhimu tu katika kuwa hai bali pia ni jambo la kuburudikia! Kwa sababu kula huwa burudani, watu wengi hukata kauli kwamba mambo yenye burudani duniani (ngono, uhusiano wa kifamilia, n.k.) yatakuwepo mbinguni. Ingawa Biblia haitupi jibu la kina kwa swali la kula chakula mbinguni, mambo machache kutoka katika Maandiko yanafaa.

Inapendeza kuona kwamba wakati Bwana Yesu alipoadhimisha Pasaka pamoja na wanafunzi wake muda mfupi kabla ya kusulubiwa kwake, alirejelea kula na kunywa katika ufalme. “Amin, nawaambia, sitakunywa tena katika uzao wa mzabibu, hadi siku ile nitakapounywa mpya katika Ufalme wa Mungu” (Marko 14:25). Ufalme wa kidunia wa milenia hakika unarejelewa hapa, na katika ufalme huo, wote ambao ni wafuasi Wake watakuwa tayari wamepokea miili yao ya ufufuo. Ingeonekana kutokana na kauli hii kwamba sisi, katika miili yetu tukufu, tutakula na kunywa katika ufalme wa milenia. Lakini vipi kuhusu ufalme wa mbinguni?

Mtume Yohana alipopewa maono ya Yerusalemu Mpya, alionyeshwa “mto wa maji ya uzima, maangavu kama kioo yakitiririka kutoka kwenye kile kiti cha enzi cha Mungu na cha Mwana-Kondoo, kupitia katikati ya barabara kuu ya huo mji. Kwenye kila upande wa huo mto kulikuwa na mti wa uzima utoao matunda ya aina kumi na mbili, ukizaa matunda yake kila mwezi. Nayo majani ya mti huo ni kwa ajili ya uponyaji wa mataifa. Katika mji huo hakutakuwa tena na laana…” (Ufunuo 22:1-3). Andiko hilo halisemi ikiwa kweli tutakula tunda la mti wa uzima, lakini hilo linawezekana kwa hakika.

Ikiwa tutakula mbinguni, hatujui kwa hakika chakula cha mbinguni kinaweza kuwa na nini, ingawa imependekezwa kwamba labda mlo wetu utakuwa kama ule wa Adamu na Hawa katika paradiso kabla ya anguko. “Kisha Mungu akasema, Nimewapa kila mche utoao mbegu juu ya uso wa dunia yote, na kila mti wenye matunda yenye mbegu ndani yake. Vitakuwa chakula chenu” (Mwanzo 1:29).

Hatimaye, hatujui ikiwa tutakula, au ni nini tutakula mbinguni. Waumini “wanajua kwa sehemu tu” 1 Wakorintho 13:9). Furaha ya kuwa pamoja na Mwokozi wetu milele, ambaye ni Mkate wa Uzima ni zaidi ya uwezo wetu mdogo wa kufahamu, kwa kuwa “bado haijadhihirika tutakavyokuwa, lakini twajua ya kwamba yeye atakapodhihirishwa, tutafanana naye, kwa maana tutamwona kama alivyo. Kila mmoja mwenye matumaini haya ndani yake hujitakasa, kama vile yeye alivyo mtakatifu” (1 Yohana 3:2-3).

English



Rudi kwa ukurasa wa nyumbani wa Kiswahili

Je! Tutakula chakula mbinguni?
Shiriki ukurasa huu: Facebook icon Twitter icon Pinterest icon Email icon
© Copyright Got Questions Ministries