settings icon
share icon
Swali

Je! Ni dhambi kutoraka na mchumba bila idhini?Biblia inasema nini kuhusu kutoroka

Jibu


Kuhala ni kutoroka kwa siri; katika muktadha wa ndoa, kutoroka husababisha harusi ambayo kawaida hufanywa bila idhini ya wazazi. Kutoroka na mchumba sio sawa na kuwa na harusi ya kibinafsi. Kutoroka kwa kawaida, lakini sio kila wakati, kunamaanisha kitu kilichokatazwa kama sababu ya usiri. Katika miaka ya hivi majuzi, neno kuhala limebadilika na kumaanisha “kupanga harusi ndogo au ile ambayo orodha ya waalikwa ni watu wachache.” Hata hivyo, kwa madhumuni ya makala hii, tutafasili kuhala kuwa “tendo la kutoroka ili kuoa kisiri,” na tutachunguza ikiwa Biblia ina lolote la kusema kuhusu hilo.

Desturi zimebadilika kwa karne nyingi na bado zinatofautiana kutoka kwa tamaduni hadi tamaduni. Katika historia ya awali ya mwanadamu, bibi na bwana walichaguana tu na kuanzisha jamii mpya (Mwanzo 2:22). Lakini, watu walipongezeka duaniani, kuunda familia mpya ilikuwa jambo la kusherehekea. Dokezo la kwanza katika Maandiko la desturi ya ndoa ni wakati Ibrahimu alipomtuma mtumishi wake kurudi katika nchi yake ili kumtafutia mwanawe Isaka mke (Mwanzo 24:3-4). Mtumishi alimwomba Bwana amwelekeze kwa msichana sahihi, na akampata Rebeka (Mwanzo 24:5-51). Familia yake ilimruhusu kufanya uamuzi, na alikubali kurudi na mtumishi na kuwa mke wa Isaka (Mwanzo 24:57-58). Hakuna kinachosemwa kuhusu harusi. Alimfuata tu mgeni katika nchi ya mbali na akawa mke wa mtu ambaye hajawahi kukutana naye.

Dokezo lingine la desturi za ndoa ni wakati Yakobo alipomkimbia kaka yake Esau mwenye hasira (Mwanzo 27:41), hadi kwa watu wa mama yake. Alipofika kwa mjomba wake Labani, Yakobo alimpenda binamu yake Raheli mara moja (Mwanzo 29:18). Labani alimtaka Yakobo kufanya kazi kwa miaka saba kama mahari ya Raheli (Mwanzo 29:20). Yakobo alikubali jambo hili—hakutoroka na Raheli— lakini, siku ya arusi ilipofika, Labani alibadilisha bibi-arusi na kumpa Yakobo binti yake mkubwa, Lea, akisema, “Si desturi yetu kumwoza binti mdogo kabla ya kumwoza binti mkubwa.” Kwa hivyo mila ya harusi ilikuwa tayari inatumika wakati huo, kumaanisha kwamba kutoroka haikuwa kawaida.

Mungu aliumba ndoa. Katika bustani ya Edeni, Alimleta Hawa kwa Adamu na kuwaunganisha pamoja kama mume na mke katika harusi ya kwanza (Mwanzo 2:21-24). Sikuzote ndoa imekuwa ya maana sana kwa Mungu na hivyo inafaa kusherehekewa. Sababu moja anachukia talaka ni kwamba Bwana mwenyewe ni shahidi kwa kila ndoa (Malaki 2:14). Katika siku za Yesu, harusi zilikuwa sherehe kubwa sana, mara nyingi zilidumu kwa zaidi ya juma moja kwa karamu na dansi. Wazo la kutoroka lingekuwa geni kwa tamaduni kama hiyo.

Kutoroka kisiri na mchumba kunadokeza kiasi cha kutokubalika kwa upande wa familia. Sababu za kawaida za kutoroka ni kuepuka aibu ikiwa bi-arusi tayari ni mjamzito, kukwepa kutokubaliwa na wazazi, au kuepuka shughuli zote za sherehe nyingi za harusi. Walakini, wanandoa wengi ambao waliotoroka baadaye wanajuta ukosefu wa picha na kumbukumbu. Mara nyingi wanahisi waliwaibia marafiki na familia zao fursa ya kushiriki katika siku yao ya furaha. Kwa sababu kutoroka kwa kawaida hakujumuishi ushiriki wa wazazi, inaonekana kukiuka amri za Biblia zinazorudiwa mara kwa mara za kuheshimu baba na mama (Waefeso 6:2; Kutoka 20:12).

Huenda kukawa na hali ambazo wenzi wa ndoa Wakristo wanataka kuoana, lakini, kwa sababu wazazi wao wako katika dini ya uwongo au wazazi wanatamani kumwoza mtoto wao kwa mtu mwingine, huenda wenzi hao wa ndoa wakaona kutoroka kuwa njia pekee. Lakini maamuzi kama hayo yanapaswa kufanywa tu wakati majaribio mengine yote ya kushirikiana na kukata rufaa kwa wazazi yamekamilika.

Kwa sababu ya kusisitizwa kwa sherehe za arusi katika Biblia, kutoroka hakuonekani kuwa chaguo la Mungu kwa wenzi wanaofunga ndoa. Kanisa linalinganishwa na bi-arusi, na Yesu ndiye Bwana-arusi (Marko 2:19-20; 2 Wakorintho 11:2). Marejeleo ya muungano huu wa siku zijazo yanaelezewa kuwa ya furaha, mzuri, na ya hadharani, sio siri. Marejeleo yote ya harusi katika historia yote ya Biblia yalihusisha sherehe kubwa na heshima kwa familia zilizoungana. Ingawa kutoroka si dhambi yenyewe, wanandoa wanapaswa kufikiria kwa makini sababu za kutaka kutoroka. Ikiwa msukumo unajumuisha vipengele vya uasi, madharau, au aibu, kutoroka kunaweza kufanya mambo kuwa mabaya zaidi. Ndoa ni muhimu sana kuanza hivyo. Inastahili heshima ya sherehe.

English



Rudi kwa ukurasa wa nyumbani wa Kiswahili

Je! Ni dhambi kutoraka na mchumba bila idhini?Biblia inasema nini kuhusu kutoroka
Shiriki ukurasa huu: Facebook icon Twitter icon Pinterest icon Email icon
© Copyright Got Questions Ministries